Ajenda muhimu za uchumi katika ziara ya Obama barani Afrika

Monday, July 1, 2013

Rais wa Senegal, Macky Sall akimkaribisha Rais wa Marekani, Barack Obama katika Ikulu ya Dakar, Alhamisi iliyopita. Kushoto ni mke wa Obama, Michelle. Picha na AFP. 

Sera ya Mpango wa Rais wa Kupambana na Malaria na HIV/AIDS (PEPFAR) ulibuniwa wakati wa Rais  George W Bush na umeendelea kwa misingi hiyo wakati wa Rais Obama na ziara yake hii italenga zaidi eneo hilo.
Ujio wa Rais Barack Obama barani Afrika kwa mara ya pili, na safari hii akikaa barani humu kwa takriban wiki moja, ni hatua inayongojewa kwa shauku kubwa, lakini ambayo wafuatiliaji wa habari na wataalamu wa uhusiano kati ya Afrika na Marekani wanashindwa kusema nini hasa cha kutegemea.
Tofauti na ziara ya Rais Xi Jinping wa China hivi karibuni, tena aliyofanya akianza kuingia madarakani - ya kwanza duniani kuacha safari tangulizi ya Russia, ‘mtalaka’ wa China katika sera za Kikomunisti za karne iliyopiga, ziara ya Obama haina matazamio ya miradi mikubwa ya ujenzi, uwekezaji au vinginevyo. Ni wazi Afrika ni muhimu zaidi kwa China hivi sasa kuliko ilivyo kwa Marekani na itabaki hivyo.
Wanaofuatilia takwimu za biashara wanasema kuwa China imeshaipiku Marekani na nchi za Ulaya kama mshirika mkuu wa biashara na Afrika, ila Ulaya ikiungwa pamoja kama Umoja wa Ulaya (EU) bado ina biashara kubwa zaidi na Afrika kuliko China.
Marekani kwa maana hiyo ni ya tatu, lakini ni ya pili kwa nchi moja moja, ingawa umuhimu wake kwa nchi za Afrika una mapana zaidi ya jinsi hizo takwimu zinavyoonyesha.
Nchi hiyo ina hisa takriban asilimia 25 ya vyombo vya fedha vya kimataifa, hasa Benki ya Dunia na Shirika la Fedha la Kimataifa, kwa hiyo uhusiano wake na Afrika kwa sehemu kubwa unakwenda kimya kimya, kama sehemu ya kazi za taasisi za kimataifa, si moja kwa moja kama uhusiano
bayana.
Ukilinganisha na China, tofauti kubwa kati ya Marekani na China kwa Afrika na ndiyo tofauti inayoonekana katika ziara za viongozi wakuu wa nchi hizo barani Afrika, ni kuwa uhusiano na China ni wa kimkataba na biashara ya ana kwa ana. Uhusiano na Marekani  una mizizi katika mifumo ya biashara iliyopo duniani na sera zake zinajulikana, hivyo unaweza kusoma mapitio na majadiliano kadhaa kuhusu ujio wa Rais Obama barani Afrika usione chochote kuhusu uhusiano huo. Sababu ni kuwa hayaamuliwi katika ziara kama hizi, ila ni sehemu ya usawiri-mifumo ya biashara kimataifa, mielekeo ya kisera inayofuatiliwa na mashirika ya Umoja wa Mataifa (UN) na mifumo ya kudumu inayokubaliwa na Bunge la Marekani.
Wakati kinachotajwa ni mikopo ya China kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu, ni rahisi kusahau kuwa mwelekeo wa kukuza uchumi kwa mauzo ya nje kumeinuliwa sana na sheria ya Marekani ya AGOA (African Growth and Opportunity Act) ambayo kwa miaka 10 sasa imekuwa ufunguo wa nchi kuingia katika soko hilo. Tofauti kati ya nchi imetokana na viwango vya ufanisi ndani ya nchi husika, na hapo ndipo zinapoonekana tofauti kati ya wale wanaotazamia mengi sana kwa ujio wa Rais Obama, na wale wanaotumia mifumo iliyopo ya biashara na Marekani.
Kwa mfano, Kenya inauza mara kumi au zaidi katika soko hilo ukilinganisha na Tanzania, ila ziara ya Obama ni kwa Tanzania na siyo Kenya; yupi mshirika halisi?
Mwelekeo wa Marekani katika biashara na Afrika unatofautiana na China kimsingi kwa sababu Marekani imejikita katika kuboresha uwezo wa Afrika kufanya biashara na kuvuta mitaji, ambayo itaboresha uwezo wa uzalishaji, ufanisi katika sekta tofauti, na upana zaidi wa sayansi na teknolojia. Marekani haitofautiani na Ulaya katika suala hilo ingawa Ulaya imechukua muda kuoanisha ushirikiano na Afrika katika mifumo ya kimataifa ya biashara kwa jumla, wakati Marekani ndiye mlinzi halisi wa mifumo hiyo.
Hivyo Umoja wa Ulaya unachukua muongo mmoja kujadiliana na Afrika nini cha kufanya baada ya uhusiano maalumu ya mkataba wa Lome kuanzia mwaka 1973 yalipoisha kwa shinikizo la Marekani mwaka 2007.
Marekani kwa upande wake haina muda wa kufanya milolongo ya mijadala na nchi za Afrika kupambanua sera zake, bali inaunda sera ndani ya michakato ya sera za vyama vya Republican na Democratic, na kwa jumla ikishaundwa sera inakuwa ya kitaifa, haibadiliki Serikali ya chama kingine ikiingia madarakani.

Kwa mfano, sera ya AGOA ilibuniwa wakati wa Rais Bill Clinton kabla ya George W. Bush kuingia madarakani mwaka 2001 mwanzoni, na haikubadilishwa lolote wakati wa utawala huo.
Kwa upande wa pili, sera ya Mpango wa Rais wa Kupambana na Malaria na HIV/AIDS (PEPFAR) ulibuniwa wakati wa Rais Bush na umeendelea kwa misingi hiyo wakati wa Rais Obama, na ziara yake hii italenga zaidi eneo hilo.
Kabla ya Obama kuingia madarakani, kwa kipindi kirefu hasa baada ya Afrika kufutiwa baadhi ya madeni yake na mengine kuingizwa katika programu za malengo ya maendeleo ya milenia, watalamu wa Afrika (kupitia mashirika tofauti ya kimataifa) walikuwa wanalilia ‘Marshall Plan’ ya Afrika.  Ni mpango ambao aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, George C. Marshall, aliyekuwa mmoja wa majenerali wake wakuu wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia, alibuni kuhusiana na Ulaya. Afrika imelilia mpango kama huo ikidhania kuwa suala hapo ni fedha tu.
Dhana kuwa mpango kabambe wa kusaidia maendeleo ya Afrika utawezesha kulivusha bara hilo kutoka umaskini na maisha ya vijijini kuingia katika viwanda na maisha ya mijini ni potofu.  Ndivyo, pamoja na kuwa hapajawahi kuwepo mpango wa mara moja wa dola bilioni 500 labda kwa dola za sasa (walivyokuwa wakisema wataalamu wa Afrika miaka 10 au 15 iliyopita).
Takwimu za Marekani za  mwaka 1947  zinaonyesha kuwa wakati mpango huo unabuniwa, nchi hiyo ilikuwa na uzalishaji wa jumla  wa thamani ya dola bilioni 258, na ilitoa dola bilioni 13 baada ya vita kumalizika, na dola bilioni 13 nyingine kwa ajili ya misaada ya kiuchumi na kiufundi, kama sehemu ya mpango huo wa Marshall.  Haikuwa ni suala la kuijaza Ulaya kifedha; vizuizi vya biashara viliondolewa na kuweka msingi wa kile ambacho baadaye kiliitwa Soko la Pamoja la Ulaya na mwishowe Umoja wa Ulaya, kuweka misingi ya amani, utawala bora na maendeleo bara lote.
Kimsingi,  hii ndiyo sera iliyotumika kote duniani kuinua nchi tofauti kutoka katika majivu na magofu ya Vita Kuu ya Pili na mifarakani mingine iliyofuata, kuingia katika maendeleo endelevu ambayo hayafuatwi na mikasa au milipuko ya kisiasa ndani ya nchi.
Wakati nchi za Afrika zinaelekea kufikia uhuru mwelekeo wao wa fikra haukuwa na mpangilio huo, kwani ziliungwa mkono na nchi za kijamaa, au za kikomunisti dhidi ya wakoloni, hivyo wakajenga hisia kuwa Ulaya na Marekani zina nia ya kuwadhulumu, na kuwatawala ikiwezekana. Hisia hiyo ilioana vyema na matakwa ya tabaka tawala baada ya uhuru lililokuwa na nia ya kuzuia mali kuingia mikono ya wageni kwa njia ya utandawazi (uhuru wa kununua hisa za makampuni, na kutokuwapo sekta kubwa inayomilikiwa na serikali katika nyanja tofauti za uchumi, n.k.) Ni sababu maendeleo kutokuwa endelevu Afrika.

0 comments:

Post a Comment

SOCIAL NETWORKS

twitterfacebookgoogle pluslinkedinrss feedemail

SEARCH IN THIS BLOG

JOIN ME ON FACEBOOK

BLOG FOLLOWERS

BLOG ACHIEVES

ADVERTISEMENT

ADVERTISEMENT

POPULAR NEWS

Je mtandao huu umekusaidia kujifunza na kupata maarifa Mapya...?